Tuesday, August 5, 2014

BUNGE MAALUMU HALIJAUZULIWA NA WAJUMBE WA UPINZANI, HUKU MWENYEKITI AKILIFUNGUA BUNGE HILO.Soma zaidi

Karibuni tena Dodoma Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge Maalum la kutunga Katiba ya nchi yetu. Sote tuna kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu wetu kwa kuendelea kutupa uhai na afya hadi leo kutuwezesha kuwepo ndani ya ukumbi huu. Tupo humu ili tuitekeleze kazi waliyotukabidhi Watanzania wenzetu milioni arobaini na sita (46) ya kuwapatia Katiba mpya. Dhamana hii ni nzito na haistahili kufanyiwa ajizi.

Tunaendelea na shughuli zetu za Bunge Maalum kwa kuzingatia Kanuni ya 30 (1) inayosema
Akidi kwa kila kikao cha Bunge Maalum isipokuwa wakati wa kupitisha uamuzi wa Bunge Maalum itakuwa ni nusu ya Wajumbe wote wa Bunge Maalum“.
Nimetaarifiwa na Katibu kwamba wajumbe waliokuja Dodoma kuhudhuria ni zaidi ya robo tatu ya Wajumbe wote wa Bunge Maalum. Nawashukuruni nyote kwa kuja hapa Dodoma ili kutimiza wajibu wenu.
Kwa niaba yenu, nawashukuru Watanzania wenzetu wote ambao kwa mamilioni wamedhihirisha utashi mwema wa kisiasa kwa kuunga mkono hatua ya Bunge Maalum kuendelea na kazi zake hadi tuipate Katiba inayopendekezwa ambayo wataipigia kura ya maoni. Kipekee na kwa niaba yenu, nawashukuru kwa dhati viongozi wetu wa dini wa madhehebu yote wanaloliombea Taifa hili mafanikio Bunge Maalum, wakitanguliza utaifa pamoja na amani ya nchi na umoja ndani ya nchi na siyo ubinafsi na maslahi ya makundi.
 Kwa leo sikupenda sana kuzungumzia hoja mbali mbali zinazotawala magumzo ya mchakato wa Katiba mpya hapa nchini, magumzo yanayoendeshwa na makundi maalum kwa jazba na hata matusi. Hata hivyo nalazimika kutoa maelezo ya ufafanuzi kuhusu upotoshaji mkubwa unaoendeshwa na baadhi ya watu kuhusu Bunge Maalum. Nikiwa Mwenyekiti wenu ninao wajibu wa kuwafafanulia wananchi kuhusu uhalali wa shughuli za Bunge Maalum linaloendelea na utaratibu wa shughuli zetu.
Ni Rasimu ya Tume au la
Wapo wanaodai kuwa eti hapa Bungeni hatujadili Rasimu ya Tume. Tuhuma hii haina ukweli hata kidogo. Msingi wa majadiliano yote tangu tumeanza ni Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Katiba. Utaratibu ni kwamba pale ambapo wajumbe wanaona panafaa kurekebishwa wanafanya hivyo. Maana ya rasimu ni andiko ambalo halijajitosheleza bila kupata ithibati ya taasisi ya juu zaidi. Anayekabidhiwa rasimu anayo haki na mamlaka ya kuirekebisha. Vinginevyo kujadili rasimu hakuna sababu. Itakuwa ni jambo la ajabu na lisilo na mantiki yoyote kuwa taasisi iliyopewa mamlaka ya kujadili Rasimu ikishaijadili iiache ibaki kama ilivyokuwa wakati ilipowasilishwa!
 Je suala ni muundo wa Muungano tu?
Maudhui ya Rasimu yanajumuisha baadhi ya masuala muhimu yafuatayo:
-      Kuimarisha Muungano wetu kwa kuleta uwiano     bora zaidi wa mamlaka ya Zanzibar na Tanzania      Bara ndani ya Muungano
-      Kuimarisha haki za binadamu ili kuwawezesha      raia wa kawaida kufaidi uhuru wa demokrasia     bila ubabe na dhuluma
-      Kuzuia wachache kufuja rasilimali za taifa bila       kujali maslahi ya wengi na ya vizazi vijavyo.
-      Kujenga uwiano sahihi na wenye haki baina ya      wanawake na wanaume katika nafasi za uongozi.
-      Kubainisha hatua zenye kuleta matumaini mapya ya maendeleo kwa makundi maalum ya vijana     wakulima wadogo, wafugaji, wafanyakazi wa ngazi   za kawaida, walemavu, wafanya biashara wadogo   na wajasiriamali wengine.
-      Kuweka msingi imara wa kutungwa kwa sheria      kakamavu za kuzuia ukandamizaji wa raia,        unyonyaji, wizi wa mali ya umma, rushwa,    hujuma dhidi ya uchumi na kuzuia mapato        haramu na fedha chafu.
-      Kutambua haki za ardhi kwa wakulima, wafugaji    na wajasiriamali wengine ili kupunguza migongano na migogoro.
-      Kuweka Misingi ya utawala bora inayozingatia        uadilifu, sifa stahiki na ufanisi.
-      Kuwezesha kutungwa kwa sheria bora zaidi     zitakazosimamia chaguzi zilizo za haki na huru    zaidi pamoja na kuwepo Tume za Uchaguzi       zilizoboreshwa.
Zaidi ya hivyo, yapo mapungufu katika Rasimu iliyopo kwa kuachwa masuala ya kuwezesha Serikali za mitaa; kutoa maelekezo kuhusu masuala ya matumizi ya ardhi na rasilimali nyingine za Taifa. Nini kinatuzuia kuiboresha Rasimu kwa kuyaongeza mambo haya ndani ya Katiba kwa faida ya Taifa?

No comments:

Post a Comment