
Karibuni
tena Dodoma Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge Maalum la kutunga Katiba ya
nchi yetu. Sote tuna kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu wetu kwa
kuendelea kutupa uhai na afya hadi leo kutuwezesha kuwepo ndani ya
ukumbi huu. Tupo humu ili tuitekeleze kazi waliyotukabidhi Watanzania
wenzetu milioni arobaini na sita (46) ya kuwapatia Katiba mpya. Dhamana
hii ni nzito na haistahili kufanyiwa ajizi.
Tunaendelea na shughuli zetu za Bunge Maalum kwa kuzingatia Kanuni ya 30 (1) inayosema
“Akidi
kwa kila kikao cha Bunge Maalum isipokuwa wakati wa kupitisha uamuzi wa
Bunge Maalum itakuwa ni nusu ya Wajumbe wote wa Bunge Maalum“.
Nimetaarifiwa
na Katibu kwamba wajumbe waliokuja Dodoma kuhudhuria ni zaidi ya robo
tatu ya Wajumbe wote wa Bunge Maalum. Nawashukuruni nyote kwa kuja hapa
Dodoma ili kutimiza wajibu wenu.
Kwa
niaba yenu, nawashukuru Watanzania wenzetu wote ambao kwa mamilioni
wamedhihirisha utashi mwema wa kisiasa kwa kuunga mkono hatua ya Bunge
Maalum kuendelea na kazi zake hadi tuipate Katiba inayopendekezwa ambayo
wataipigia kura ya maoni. Kipekee na kwa niaba yenu, nawashukuru kwa
dhati viongozi wetu wa dini wa madhehebu yote wanaloliombea Taifa hili
mafanikio Bunge Maalum, wakitanguliza utaifa pamoja na amani ya nchi na
umoja ndani ya nchi na siyo ubinafsi na maslahi ya makundi.
Kwa
leo sikupenda sana kuzungumzia hoja mbali mbali zinazotawala magumzo ya
mchakato wa Katiba mpya hapa nchini, magumzo yanayoendeshwa na makundi
maalum kwa jazba na hata matusi. Hata hivyo nalazimika kutoa maelezo ya
ufafanuzi kuhusu upotoshaji mkubwa unaoendeshwa na baadhi ya watu kuhusu
Bunge Maalum. Nikiwa Mwenyekiti wenu ninao wajibu wa kuwafafanulia
wananchi kuhusu uhalali wa shughuli za Bunge Maalum linaloendelea na
utaratibu wa shughuli zetu.
Ni Rasimu ya Tume au la
Wapo
wanaodai kuwa eti hapa Bungeni hatujadili Rasimu ya Tume. Tuhuma hii
haina ukweli hata kidogo. Msingi wa majadiliano yote tangu tumeanza ni
Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Katiba. Utaratibu ni kwamba
pale ambapo wajumbe wanaona panafaa kurekebishwa wanafanya hivyo. Maana
ya rasimu ni andiko ambalo halijajitosheleza bila kupata ithibati ya
taasisi ya juu zaidi. Anayekabidhiwa rasimu anayo haki na mamlaka ya
kuirekebisha. Vinginevyo kujadili rasimu hakuna sababu. Itakuwa ni jambo
la ajabu na lisilo na mantiki yoyote kuwa taasisi iliyopewa mamlaka ya
kujadili Rasimu ikishaijadili iiache ibaki kama ilivyokuwa wakati
ilipowasilishwa!
Je suala ni muundo wa Muungano tu?
Maudhui ya Rasimu yanajumuisha baadhi ya masuala muhimu yafuatayo:
- Kuimarisha Muungano wetu kwa kuleta uwiano bora zaidi wa mamlaka ya Zanzibar na Tanzania Bara ndani ya Muungano
- Kuimarisha haki za binadamu ili kuwawezesha raia wa kawaida kufaidi uhuru wa demokrasia bila ubabe na dhuluma
- Kuzuia wachache kufuja rasilimali za taifa bila kujali maslahi ya wengi na ya vizazi vijavyo.
- Kujenga uwiano sahihi na wenye haki baina ya wanawake na wanaume katika nafasi za uongozi.
-
Kubainisha hatua zenye kuleta matumaini mapya ya maendeleo kwa makundi
maalum ya vijana wakulima wadogo, wafugaji, wafanyakazi wa ngazi
za kawaida, walemavu, wafanya biashara wadogo na wajasiriamali
wengine.
-
Kuweka msingi imara wa kutungwa kwa sheria kakamavu za kuzuia
ukandamizaji wa raia, unyonyaji, wizi wa mali ya umma, rushwa,
hujuma dhidi ya uchumi na kuzuia mapato haramu na fedha chafu.
- Kutambua haki za ardhi kwa wakulima, wafugaji na wajasiriamali wengine ili kupunguza migongano na migogoro.
- Kuweka Misingi ya utawala bora inayozingatia uadilifu, sifa stahiki na ufanisi.
-
Kuwezesha kutungwa kwa sheria bora zaidi zitakazosimamia chaguzi
zilizo za haki na huru zaidi pamoja na kuwepo Tume za Uchaguzi
zilizoboreshwa.
Zaidi
ya hivyo, yapo mapungufu katika Rasimu iliyopo kwa kuachwa masuala ya
kuwezesha Serikali za mitaa; kutoa maelekezo kuhusu masuala ya matumizi
ya ardhi na rasilimali nyingine za Taifa. Nini kinatuzuia kuiboresha
Rasimu kwa kuyaongeza mambo haya ndani ya Katiba kwa faida ya Taifa?
No comments:
Post a Comment